}

SERIKALI YAWEKA MIKAKATI KUBORESHA MIUNDOMINU YA SHULE

Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM)  na Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari  (MMES)  imeendelea kuboresha na kurekebisha miundo mbinu katika shule za msingi na sekondari nchini ili kufikia azma ya kutoa elimu bora kwa Watanzania.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. George Simbachawene alipokuwa akizungumzia mikakati ya Serikali katika kuboresha miundo mbinu ya shule za msingi na sekondari.
“Kupitia programu za MMEM na MMES, Serikali inaendelea kujenga, kukarabati, na kuimarisha miundo mbinu katika shule zake hapa nchini kwa manufaa ya watoto wetu na taifa kwa ujumla” alisema Simbachawene

Simbachawene alisema kuwa changamoto kubwa zipo katika shule za msingi hali inayotokanana na sera ya elimu bure ambapo kumekuwa na ongezeko kubwa la uandikishaji wa wanafunzi wanaojiunga na shule za msingi. Ongezeko hilo linapelekea miundombinu mingi kupungua ikilinganishwa na idadi ya wanafunzi.

Changamoto hizo ni pamoja na upungufu wa madarasa, matundu ya vyoo na nyumba za walimu.
Katika kulipatia ufumbuzi suala hilo, Simbachawene alitaja baadhi ya Mikakati kuwa ni kuimarisha miundombinu na kuziagiza Halmashauri zote nchini kuongeza bajeti ya elimu katika bajeti ya  mwaka jana  2016/17.

“Halmashauri zilielekezwa kutoa kipaumbele katika miundombinu ya shule ili kuwa na mazingira rafiki kwa walimu na wanafunzi kwa kufundishia na kujufunzia ambayo yatapelekea ufaulu mzuri” Aliongeza Simbachawene.

Aidha, kuhusu ukosefu wa matundu ya vyoo , Simbachawene alisema suala hilo kwa sasa halipo kwa sababu sera ya elimu inasema kuwa shule isiyokuwa na vyoo ni lazima ifungwe, na alitoa agizo katika kikao alichofanya hivi karibuni na wataalamu kuwa kila shule inapojengwa ni lazima iwe na vyoo venye hadhi na nyumba za walimu ambazo angalau zina samani muhimu.

Alitoa wito kwa wananchi kuchangia maendeleo ya shule kwa sababu shule hizo ni mali yao, kutokana na ugatuzi wa madaraka ambapo shule hizo zipo chini ya mamlaka ya Serikali za Mitaa , na kufanya umiliki wa shule kuwa mikononi mwa wananchi. 

No comments

Haki zimehifadhiwa. Copyright, kituochahabari.com ©2016. Blog designed by Geofrey Donatus Jacka.. Powered by Blogger.