}

Jamal Malinzi wakutana uso kwa uso na Zahoro Pazi wa Mbeya City, Wamezungumzia haya.

Jamal Malinzi (kushoto)  na Zahoro Pazi wa Mbeya City. 

MSHAMBULIAJI wa Mbeya City, Zahoro Pazi leo Jumatatu amekutana na Rais wa Shirikisho la Soka nchini (TFF), Jamal Malinzi kwa ajili ya kujadiliana juu ya tatizo lake la kuzuiwa kwa ITC yake na timu ya FC Lupopo ya DR Congo.

Wiki iliyopita Zahoro, alimtumia ujumbe Rais huyo ili aweze kuona ni namna gani atamsaidia upatikanaji wa ITC ili aweze kuichezea Mbeya City.

Katika ujumbe huo, Zahoro alimweleza wazi Malinzi kuwa ITC yake ilitolewa na Boniface Wambura (Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya ligi) bila idhini yake huku yeye akidai kuwa hajawahi kusaini mkataba na Lupopo kwani makubaliano yao hayakufikiwa.

Kikao hicho ambacho kimefanyika katika hoteli ya Break Point, Kinondoni kilimuhusisha pia baba mzazi wa Zahoro, Idd Pazi na mwakilishi wa Mbeya City, Mohamed Mashango.

Habari kutoka ndani ya kikao hicho zimeelezea kwamba Malinzi ameahidi kushughulikia tatizo hilo ambapo ametoa muda wa siku saba kuanzia leo kuwa ITC yake itakuwa imepatikana.

Zahoro ameanza kushughulikia ITC yake miaka miwili iliyopita lakini juhudi zake zilikuwa zikigonga mwamba kutokana na kukosa nguvu ya kusaidia kutoka TFF huku Lupopo wakisisitiza kuwa ni lazima arejeshe pesa aliyochukuwa wakati anasaini mkataba huo hewa.

Mshambuliaji huyo hajacheza ligi kwa miaka yote miwili ingawa aliwahi kupata timu ya Polisi Moro pamoja na African Sports lakini kucheza kwake ilikuwa ni vigumu.

No comments

Haki zimehifadhiwa. Copyright, kituochahabari.com ©2016. Blog designed by Geofrey Donatus Jacka.. Powered by Blogger.