}

HAZINA SACCOSS WASISITIZWA KUWAFIKIA WATUMISHI WA UMMA WENGI ZAIDI.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Rosemery Staki Senyamule, ametoa wito kwa uongozi wa Chama cha Akiba na Mikopo cha HAZINA (HAZINA SACCOS), kuongeza kasi ya kutoa elimu kwa watumishi wa umma ili wajiunge na Mfuko huo na kunufaika na fursa zinazotolewa ili kuwawezesha kuboresha maisha yao.

Mhe. Senyamule ametoa rai hiyo jijini Dodoma wakati alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha kwenye Maonesho ya Nanenane Kitaifa yanayofanyika katika Viwanja vya Nanenane, Nzuguni, Jijini Dodoma, yenye kauli mbiu “Chagua Viongozi Bora kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo na Uvuvi 2025. 

"Watumishi wengi bado hawana uelewa wa kutosha kuhusu faida za kujiunga na HAZINA Saccos hivyo ni jukumu lenu kuhakikisha elimu hii inawafikia wengi iwezekanavyo, ili nao waweze kujiunga na Saccos hii," alisema Mhe. Senyamule.
Aliishauri Hazina Saccos kutumia mbinu mbalimbali za utoaji elimu, ikiwemo mikutano ya hadhara, matangazo ya redio na televisheni, pamoja na mitandao ya kijamii ili kufikia idadi kubwa ya watumishi ili waweze kujikwamua kiuchumi kupitia mikopo yenye masharti nafuu tofauti na taasisi zingine za kifedha.

Awali akizungumza wakati akimkaribisha Mkuu wa Mkoa kupata maelezo ya kina yanayotolewa na Saccos ya Hazina, Afisa Huduma, Bi. Leah Nkinda, alisema kuwa chama hicho kimezindua mikopo miwili mipya, ya Tuliza Moyo na Ajira Mpya, inayolenga kuwasaidia watumishi wa umma kukabiliana na changamoto za kiuchumi.

Alisema mikopo hiyo inapatikana kwa masharti nafuu ikilenga kumwezesha mtumishi wa umma kukidhi mahitaji ya dharura ambapo mikopo hiyo ni jibu kwa mikopo mingi ya mitaani inayotozwa riba kubwa, inayowakandamiza watumishi.
‘‘Mkopo wa Tuliza Moyo unatozwa bila riba na unalenga kumsaidia mtumishi kukidhi mahitaji ya dharura na mkopo huu hurejeshwa ndani ya mwezi mmoja na kiwango kinaanzia Shilingi laki tatu hadi shilingi milioni moja na hupatikana ndani ya saa 24 za kazi tangu maombi kuwasilishwa’’, alifafanua Bi.Nkinda

Aliongeza kuwa Hazina Saccos pia inatoa mkopo wa Ajira Mpya ambao umewekwa kwa ajili ya watumishi wa umma walioajiriwa ndani ya miezi sita iliyopita ikiwa na lengo la kumwezesha mtumishi huyu mpya kujikimu kimaisha huku akianza safari yake ya utumishi wa umma.

Wizara ya Fedha pamoja na Taasisi zilizo chini yake inashiriki katika Maonesho ya Nanenane Kitaifa katika Viwanja vya Nanenane, Jijini Dodoma, yenye kauli mbiu “Chagua Viongozi Bora kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo na Uvuvi 2025’’.


No comments

Haki zimehifadhiwa. Copyright, kituochahabari.com ©2016. Blog designed by Geofrey Donatus Jacka.. Powered by Blogger.